UTAKATIFU NI PAMOJA NA KUSALI, KUSIFU NA KUABUDU

 

SURA YA KWANZA

TUSALI KWANZA SALA YA  ASUBUHI

Kama umeanza kusoma asubuhi Sali  kwanza sala hii.

+Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.

Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu mmoja, sasa na siku zote na milele amina. Ee utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu; +Baba, +Mwana na +Roho Mtakatifu. Ninasadiki kuwa upo hapa na mahali pote.

Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristu, umenizidishia neema zako, umenitayarishia makao yangu mbinguni.

Ee Mungu wangu, nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda. Ee Mungu wangu, ninakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi na furaha, na mateso yangu, uyapokee unipe neema yako nisitende leo dhambi, Amina.

______________________

Ee Baba yetu Mungu mkuu,

Umenilinda usiku huu.

Nakushukuru kwa moyo,

Ee Baba, Mwana na Roho.

Nilinde tena siku hii,

Niache dhambi, nikutii.

Naomba sana Baba wee,

Baraka zako nipokee.

Bikira safi, Ee Maria

Nisipotee nisimamie.

Mlinzi mkuu malaika wee,

Kwa Mungu wetu niombee

Nitake nitende mema tu,

Na mwisho nije kwako juu. Amina.

NIA NJEMA.

Kumheshimu Mungu wangu

Namtolea roho yangu,

Nifanye kazi nipumzike

Amri zake tu nishike

Wazo, neno, tendo lote

Namtolea Mungu pote

Roho, mwili chote changu,

Pendo na uzima wangu

Mungu wangu nitampenda,

Wala dhambi sitatenda.

Jina lako nasifia,

Utakalo hutimia.

Kwa utii navumilia

Teso na matata pia.

Nipe, Bwana, neema zako

Niongeze sifa yako. Amina.

SALA YA MATOLEO.

Ee Yesu, kwa mikono ya Bikira Maria, na kwa maungano na sadaka yako kuu, ninakutolea sala, matendo, masumbuko na furaha zangu zote za leo. Ee Yesu, ufalme wako utufikie.

BABA YETU.

Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe. Ufalme wako ufike. Utakalo lifanyike duniani kama mbinguni.

Utupe leo mkate wetu wa kila siku. Utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini utuopoe maovuni. Amina.

SALAMU MARIA.

Salamu, Maria, umejaa neema; Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu mzao wa tumbo lako amebarikiwa.

Maria Mtakatifu mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu. Sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.

KANUNI YA IMANI.

Nasadiki kwa Mungu Baba mwenyezi. Muumba wa Mbingu na dunia. Na kwa Yesu Kristo Mwanae wa pekee, Bwana wetu. Aliyetungwa kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, akazaliwa na Bikira Maria. Akateswa kwa mamlaka ya Ponsiyo Pilato. Akasulibiwa, akafa, akazikwa, akashukia kuzimu. Siku ya tatu akafufuka katika wafu. Akapaa mbinguni, amekaa kuume kwa Mungu Baba Mwenyezi. Toka huko atakuja tena kuwahukumu wazima na wafu.

Nasadiki kwa Roho Mtakatifu, kanisa takatifu katoliki, ushirika wa watakatifu, maondoleo ya dhambi, ufufuko wa miili na uzima wa milele ijayo. Amina.

AMRI ZA MUNGU.

1. Ndimi Bwana Mungu wako, usiabudu Miungu wengine.

2. Usilitaje bure jina la Mungu wako.

3. Shika kitakatifu siku ya Mungu.

4. Waheshimu Baba na Mama upate miaka mingi na heri duniani.

5. Usiue.

6. Usizini.

7. Usiibe.

8. Usiseme uongo.

9. Usitamani mwanamke asiye mke wako.

10. Usitamani mali ya mtu mwingine.

AMRI ZA KANISA.

1. Hudhuria misa takatifu, dominika na sikukuu zilizoamriwa.

2. Funga siku ya jumatano ya majivu; usile nyama siku ya ijumaa kuu.

3. Ungama dhambi zako walau mara moja kila mwaka.

4. Pokea Ekaristi takatifu hasa wakati wa Paska.

5. Saidia kanisa katoliki kwa zaka.

6. Shika sheria katoliki za ndoa.

Ee Maria Bikira Mtakatifu, Mama wa Mungu na Mama yangu, nawe Mtakatifu Yosefu, Nawe malaika mlinzi wangu, nanyi watakatifu somo wangu, nanyi watakatifu wote, niombeeni nipate kuacha dhambi, nilindeni siku ya leo na siku zote, na saa ya kufa kwangu, Amina.

SALA YA IMANI.

Mungu wangu, nasadiki maneno yote. Linayosadiki na linayofundisha Kanisa Katoliki la Roma. Kwani ndiwe uliyetufumbulia hayo. Wala hudanganyiki, wala hudanganyi. Amina.

SALA YA MATUMAINI.

Mungu wangu, natumaini kwako, nitapewa kwa njia ya Yesu Kristo. Neema zako hapa duniani, na utukufu mbinguni. Kwani ndiwe uliye agana hayo nasi, nawe mwamini. Amina.

SALA YA MAPENDO.

Mungu wangu, nakupenda zaidi ya chochote. Kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza. Nampenda na jirani yangu, kama nafsi yangu, kwa ajili yako. Amina.

SALA YA KUTUBU.

Mungu wangu nimetubu sana, niliyokosa kwako. Kwani ndiwe mwema, ndiwe nwenye kupendeza. Wachukizwa na dhambi, basi sitaki kukosa tena. Nitafanya kitubio, naomba neema yako, nipate kurudi. Amina.

SALA KWA MALAIKA MLINZI.

Malaika mlinzi wangu, unilinde katika hatari zote, za roho na za mwili. Amina.

MALKIA WA MBINGU

Malkia wa mbingu, furahi Aleluya,

Kwani uliyestahili kumchukua Aleluya,

Amefufuka alivyosema Aleluya

Utuombee kwa Mungu Aleluya

Furahi, shangilia, Ee Bikira Maria Aleluya,

Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya.

Tuombe:

Ee Mungu uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao; fanyiza twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

Atukuzwe Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu, nikama mwanzo, sasa na siku zote na milele Amina.

Roho za waumini marehemu wapate rehema kwa Mungu wapumzike kwa amani.

Mt. Marko Mwinjili utuombee.

Kwa jina la +Baba na la +Mwana na la +Roho Mtakatifu. Amina

 

SALA KABLA YA KUPOKEA EKARISTI TAKATIFU.

IMANI

Kristu Yesu Mwokozi wangu, nasadiki upo kweli katika altare hapa. Nasadiki kwamba nitapewa sasa hivi mwili wako na damu yako pamoja na roho yako na umungu wako. Nasadiki kwani

ndiwe mwenyewe uliyetueleza.

MATUMAINI

Ee Mungu wangu umesema kwamba, watu waliokutumainia hawatadanganyika kwako. Basi nimekutumainia kwamba utatimiza maagano uliyoagana nasi, kuwa nikilishwa mwili wako duniani hapa, nitapata kufika kwako mbinguni na

kukuona milele.

KUABUDU

Yesu mwema, nakuabudu katika hostia takatifu; nakuungama ndiwe Muumba wangu na Bwana wangu;nakunyenyekea; nakutolea heshima na chochote changu.

KUTUBU

Bwana wangu, sistahili uingie kwangu, kwani mkosefu mimi, nikatenda dhambi nyingi; nawe ndiwe mwenye utakatifu kamili, wapenda utakatiu, wachukia maovu yangu. Una enzi kuu, waweza kufuta dhambi zangu kabisa. Basi nazichukia nami, nakuomba uniondolee,

unitakase kabisa, nipate kukupokea kwa moyo mwema.

MAPENDO

Ee Mungu, umejifumba katika sakramenti ya ekaristi kwa sababu umenipenda mno! Unitie moyo wa kukupenda sana, vilevile ulivyonipenda.

UNYENYEKEVU

Ee Yesu wangu, Bwana wangu, una utakatifu kamili; nami si mtakatifu kabisa, ila ni mtenda dhambi nyingi. Sistahili kweli unijie kwangu: useme neno tuu na roho yangu ipone.

KUTAMANI

Roho yangu inakutamani Mungu wangu, ndiwe mwenye kunifurahisha; ndiwe mwenye kuniletea heri. Unionee huruma, unifanyie neema kuu, uje kuniangalia, uje kukaa kwangu, nami nikae nawe. Amina.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Maoni

Machapisho Maarufu